Mkoa wa Dar es Salaam unapakana/umezungukwa na Mkoa wa Pwani kwa pande za Kaskazini, Magharibi na Kusini Magharibi. Bahari ya Hindi ndiyo mpaka wa Mkoa kwa upande wa Mashariki na Kusini Mashariki, ambapo una ufukwe wenye urefu wa km. 124. Eneo la Mkoa ni Kilomita za mraba 1,397. Kati ya eneo hilo kilomita za mraba 452 ndizo zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa Mji na 673 ni eneo linalofaa kwa kilimo na ufugaji. Aidha, kilomita za mraba 272 ni eneo la maji katika Bahari ya Hindi. |
Mkoa wa Dar es Salaam, kwa mujibu wa Sensa ya mwaka 2002, idadi ya watu ilikuwa 2,487,288 sawa na ongezeko la asilimia 4.3 kwa mwaka. Katika kipindi cha mwaka 2008, Mkoa unakisia kuwa na idadi ya watu takribani Millioni 4.5 kutokana na ongezeko la kawaida pamoja na wahamiaji wa ndani ya nchi wanaokuja kibiashara na kutafuta maisha mazuri.
Asilimia 65.1 ya wakazi wana umri kati ya miaka 15 – 64 na asilimia 34.9 wana umri wa miaka 0 – 14 na 65 na kuendelea. Msongamano wa watu kwa kilomita ni 2,009 mwaka 2007 (makisio). Hali inayoashiria umuhimu wa kuandaa mipango kabambe ya matumizi bora ya ardhi. |
Pato ghafi la Mkoa wa Dar es Salaam lilikuwa Sh. 1,961,505 Millioni mwaka 2005, liliongezeka hadi kufikia sh. 2,323,743 millioni mwaka 2006. Pato la mtu ni Tshs. 829,412 mwaka 2006 ambalo ni kubwa mara mbili ukilinganisha na wastani wa kitaifa wa Tshs 399,594 . Aidha Mkoa unachangia pato la Taifa kati ya asilimia 15 hadi 17 ikiwa ni kiasi kikubwa kuliko mikoa yote nchini. |
| |
|